Wananchi Geita Mji Watakiwa kwenda na kasi ya Awamu ya Tano
Mkuu wa Mkoa wa Geita Mhandisi Robert Gabriel amewataka wananchi wote na watendaji wa Halmashauri ya Mji wa Geita kuanzia ngazi ya kijiji kuendana na kasi ya Serikali ya awamu ya tano kwa kujitolea kikamilifu katika kushiriki kwenye ujenzi wa majengo ya zahanati, vituo vya afya, madarasa na nyumba za walimu ili kujiletea maendeleo katika maeneo yao na Taifa kwa ujumla.
Mkuu wa Mkoa wa Geita ametoa agizo hilo tarehe 8/5/2018 wakati wa ziara yake katika vijiji na mitaa ya Halmashauri ya Mji Geita, ambapo alizindua rasmi ujenzi wa zahanati katika Kitongoji cha nyaseke,kijiji cha Igwata, kijiji cha Gamashi katika kata ya Bulela na zahanati ya Mtaa wa Nyakahongola inayojengwa katika kata ya Kasamwa, Halmashauri ya Mji wa Geita.
Mhandisi Robert Gabriel ameagiza vijiji vyote vilivyoko katika Halmashauri ya Mji na Mkoa mzima wa Geita vyenye maeneo yaliyotengwa kwa ajili ya ujenzi wa zahanati wahakikishe ujenzi huo unaanza mapema ndani yam waka huu wa fedha. Pia amewasihi wananchi wote kufanya kazi katika sehemu ambayo Mungu amemjalia kila mmoja.
“Naagiza ujenzi wa zahanati zinazojengwa uende sambamba na ujenzi wa nyumba pacha ya watumishi wa zahanati hizo akiwemo mganga, ujenzi huu utakapokamilika mapema utawapunguzia adha ya kutembea umbali mrefu kwa wanawake na watoto ambao huwalazimu kutembea zaidi ya kilometa tano kutoka katika maeneo wanayoishi mpaka zahanati za vijiji vya jirani ili kupata huduma za matibabu.” Aliongeza Mkuu wa Mkoa wa Geita.
Mkuu wa Mkoa alitumia fursa hiyo kuwaeleza wananchi lengo la ziara yake kuwa ni kuwahamasisha wananchi katika maeneo yao kufanya kazi kwa pamoja na kutatua kero na changamoto zinazowakabili. Pia alimuagiza Mkurugenzi wa Halmashauri ya Mji wa Geita kuhakikisha mafundi watakaojenga miundo mbinu hiyo wawe ni wa kujitolea kutoka katika vijiji na mitaa husika na si kuajiri wakandarasi kutoka mikoa ya jirani ili kupunguza gharama za ujenzi na kudumisha uzalendo.
Kwa upande wake Diwani wa Kata ya Bulela Mheshimiwa Salome Kitula amewataka wananchi wake kutotegea katika kazi ya ujenzi wa zahanati na kuwaagiza watendaji wa vijiji kuwalipisha faini watu wote watakaotega katika shughuli hiyo. Kadhalika, Diwani wa Kata ya Kasamwa Mheshimiwa Mary Kasanda amesema kuwa wanakumbana na changamoto ya baadhi ya wananchi kutokuwa tayari kuchangia ujenzi wa miradi ya maendeleo katika maeneo yao.
Mkuu wa Mkoa wa Geita amezindua ujenzi huu ikiwa ni awamu ya tatu ya ziara za aina hiyo katika Halmashauri ya Mji wa Geita, ambapo Mkurugenzi wa Halmashauri ya Mji wa Geita Mhandisi Modest Apolinary amemshukuru Mkuu wa Mkoa wa Geita kwa jitihada zake za kuleta mapinduzi ya kimaendeleo kwa Mkoa wa Geita na Halmashauri ya Mji itachangia mifuko 100 kwa kila zahanati iliyoanza kujengwa. Pia amewasihi wananchi wa vitongoji vyote na vijiji vilivyoko katika maeneo yaliyozindua ujenzi kujitolea katika shughuli zote za ujenzi wa zahanati zao.
Geita Tanzania
Sanduku la Posta: P.o Box 384 Geita
Namba ya Simu: 0282520437
Mobile:
Barua pepe: td@geitatc.go.tz
Hatimiliki 2017 Halmashauri ya Mji Geita . Haki zote zimehifadhiwa