Tumieni Fursa Za Elimu Zitolewazo Na Serikali- DC
Mkuu wa Wilaya ya Geita Mheshimiwa Wilson Shimo ameiasa jamii kuhakikisha wanatumia vyema fursa ambazo zinazotolewa na Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa ajili ya kujiendeleza kielimu kuanzia ngazi ya awali, msingi hadi vyuo vikuu.
Mhe. Shimo ametoa kauli hiyo alipokuwa akizungumza na hadhara wakati wa Maadhimisho ya kilele cha juma la Elimu ya Watu wazima Wilayani Geita katika uwanja wa CCM Kalangalala hivi karibuni.
Mkuu wa Wilaya ya Geita ameeleza kuwa Serikali ya Jamhuri ya Muungano chini ya uongozi wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Samia Suluhu Hassan imeendelea kutoa nafasi za watanzania kupata elimu chini ya mfumo rasmi na nje ya mfumo rasmi, ambapo watu wazima walioshindwa kupata elimu ya msingi kwa mfumo rasmi (MEMKWA) pia wasichana waliokatisha masomo ya elimu ya sekondari kutokana na sababu mbalimbali wamerejeshwa shule.
“Ndugu wanageita wenzangu nawasihi msipuuzie nafasi hizi zilizotolewa na Serikali yetu kwa kuacha tabia ya kuwaficha ndani Watoto wenye ulemavu, hii ni kuwanyima kupata fursa ya elimu ambayo ni haki yao ya msingi. Kadhalika walimu na wazazi mnatakiwa kushirikiana kuhakikisha tatizo la utoro sugu na rejareja wa wanafunzi wa Shule za msingi na Sekondari linadhibitiwa kikamilifu”. Aliongeza Mhe. Shimo.
Akizungumzia changamoto zinazoikabili elimu ya watu wazima, Afisa Elimu ya Watu wazima Halmashauri ya Mji Geita Bi. Rahel Mwera amesema kuwa baadhi ya vikwazo vinavyochangia kuzorota kwa shughuli za elimu kwa watu wazima ni pamoja na walimu wanaofundisha madarasa ya watu wazima kutowezeshwa, wazazi kuwaficha Watoto wanaostahili kuandikishwa madarasa ya MEMKWA, mahudhurio hafifu ya wanakisomo kutokana na kusongwa na shughuli za kujitafutia mahitaji ya kujikimu kimaisha na sehemu kubwa ya wananchi kutokuwa na uelewa juu ya manufaa ya elimu ya watu wazima.
Geita Tanzania
Sanduku la Posta: P.o Box 384 Geita
Namba ya Simu: 0282520437
Mobile:
Barua pepe: td@geitatc.go.tz
Hatimiliki 2017 Halmashauri ya Mji Geita . Haki zote zimehifadhiwa