Mradi Mkubwa wa Maji Kutekelezwa Geita Mji
Halmashauri ya Mji wa Geita inataraji kupokea neema ya kupata mradi mkubwa wa maji unaotarajiwa kuanza kutekelezwa hivi karibuni.
Akiwa ziarani katika Halmashauri ya Mji Geita hivi karibuni Naibu Waziri wa Maji Mheshimiwa Juma Aweso amesema kuwa Serikali imetoa zaidi ya Dola Milioni 500 ambazo ni mkopo nafuu kutoka Serikali ya India kwa ajili ya kutekeleza Mradi mkubwa wa maji katika miji 28 Geita Mji ukiwa miongoni.
Naibu Waziri wa Maji alitoa pongezi kwa Mbunge wa Geita Mjini kwa kupigania na kuhakikisha utekelezaji wa mradi mkubwa wa maji katika Mji wa Geita na kuahidi kabla yam waka kuisha wakandarasi watakuwa katika maeneo ya kazi. “Viongozi wa Wizara ya Maji hawatokuwa kikwazo katika jitihada za Serikali kuhakikisha wananchi wanapata maji safi na salama yanayotosheleza mahitaji.”Aliongeza Mheshimiwa Aweso.
Mheshimiwa Aweso alitumia fursa hiyo kuwaagiza wataalam wa Wakala wa Maji na Usafi wa Mazingira Vijijini( RUWASA) kuhakikisha visima vilivyochimbwa havigeuki mapambo bali viwanufaishe wananchi. Pia kuanzishwa kwa RUWASA isiwe kichaka kwa wataalam wa maji kutotoa taarifa za utekelezaji kwa viongozi wa Mkoa na Wilaya katika maeneo yao pale zinapohitajika.
Kwa upande wake Mbunge wa Geita Mjini Mheshimiwa Costantine Kanyasu alitoa pongezi kwa Wizara ya Maji kwa kazi kubwa iliyofanyika kwenye mradi wa Dampo katika Mji wa Geita. Pia aliwasilisha ombi la kuunganishiwa maji katika vituo vya afya na zahanati zinazojengwa kama Nyamalembo, ambapo Naibu Waziri ameahidi baada ya kipindi kifupi ataagiza wataalam wake kufika kwa ajili ya kufanya utafiti.
Akizungumza kwa niaba ya Mwenyekiti wa Halmashauri ya Mji wa Geita Diwani wa Kta ya Kalangalala Mheshimiwa Zephania Mahushi aliomba kwa niaba ya wananchi wa Kata ya Mgusu kupatiwa huduma ya maji kutoka katika bomba kubwa la maji linalotoka Nungwe kwenda Geita mjini ambalo linapita katika kata yao lakini wao wamekuwa ni walinzi tu wa bomba hilo kwani huduma ya maji katika kata hiyo ni duni sana.
Mheshimiwa Aweso katika ziara yake ametembelea uchimbaji wa kisima kirefu katika kijiji cha Manga kata ya Mgusu ambacho kitakamilika katika mwaka wa fedha 2019/2020 na kimegharimu kiasi cha shilingi milioni 22, ujenzi wa kisima katika mtaa wa Kasamwa na ukaguzi wa kisima kilichokamilika na kinachohudumia wananchi katika kijiji cha Bulela.
Geita Tanzania
Sanduku la Posta: P.o Box 384 Geita
Namba ya Simu: 0282520437
Mobile:
Barua pepe: td@geitatc.go.tz
Hatimiliki 2017 Halmashauri ya Mji Geita . Haki zote zimehifadhiwa