Kutotumia Dawa ni Kujichimbia Kaburi – Mhe. Kanyasu
Mbunge wa Jimbo la Geita Mjini Mheshimiwa Costantine Kanyasu amewaasa watu wanaoishi na maambukizi ya Virusi vya UKIMWI kuendelea kutumia dawa zinazotolewa kwa ajili ya kufubaza makali ya virusi hivyo.
Mhe. Kanyasu ameyasema hayo Disemba mosi 2022 alipokuwa akizungumza na hadhira iliyokuwa imeshiriki maadhimisho ya siku ya UKIMWI duniani yaliyofanyika kiwilaya katika ukumbi wa shule ya Sekondari Shantamine kata ya Mtakuja.
Mbunge Kanyasu amewataka WAVIU kutoona aibu kufuata dawa kwenye vituo vya kutolea huduma za afya au kutomeza dawa kutokana na maelekezo ya waganga wa tiba asilia na viongozi wa kidini ambayo yanawaaminisha katika uponyaji wa ugonjwa walionao kwa njia ya maombezi.
“Napenda kuwatahadharisha ndugu zangu WAVIU kutopuuzia matumizi ya dawa za kufubaza makali ya VVU au kutofuata kanuni za matumizi bora ya dawa pamoja na ushauri nasaha kutoka kwa wataalam wa afya, mkifanya hivyo mtakuwa mnafupisha muda wa Maisha yenu hapa duniani kwa makusudi.” Aliongeza Mhe. Kanyasu.
Mbunge wa Geita Mjini ameahidi kuwa ataendelea kushirikiana na Halmashauri yake katika kuhakikisha elimu juu ya kujikinga na maambukizi mapya ya VVU inaendelea kutolewa katika jamii ili kufanikisha malengo ya kuondoa maambukizi mapya, vifo vitokanavyo na ugonjwa wa UKIMWI na kuondoa tatizo la unyanyapaa kwa WAVIU ifikapo mwaka 2030. Kadhalika amewakumbusha wazazi na walezi kutochoka kuzungumza na Watoto pamoja na vijana wao juu ya kuepukana na matendo maovu ambayo yanakinzana na desturi za kitanzania pia yanachochea maambukizi ya Virusi vya UKIMWI.
Kwa upande wa Mwenyakiti wa Halmashauri ya Mji Geita Mhe. Costantine Morandi amesema kuwa kila mwananchi kwa nafasi yake achukue hatua za Madhubuti kuhakikisha anapambana na kutokomeza maambukizi mapya ya VVU kwani takwimu zinaonyesha kiwango cha maambukizi katika mji wa Geita bado ni kikubwa.
Akizungumza kwa niaba ya jumuiya ya watu wanaoishi na maambukizi ya VVU wilayani Geita kwa kifupi KONGA, Ndugu Ponsian Magezi ameiomba jamii kubadili tabia kama ulevi wa kupindukia, mila za kurithi wajane, biashara za ngono ambazo jamii imezikumbatia pasipo kutambua kuwa ni hatarishi na zinachochea kasi ya maambukizi ya VVU kuongezeka.
Maadhimisho ya Siku ya UKIMWI Duniani kwa mwaka 2022 yalibeba kauli mbiu inayosema “IMARISHA USAWA” ambayo inasisitiza usawa katika maeneo yote ya utoaji wa huduma kwa kuzingatia usaa wa makundi yote pasipo kunyanyapaa hata mtu mmoja.
Geita Tanzania
Sanduku la Posta: P.o Box 384 Geita
Namba ya Simu: 0282520437
Mobile:
Barua pepe: td@geitatc.go.tz
Hatimiliki 2017 Halmashauri ya Mji Geita . Haki zote zimehifadhiwa