Geita, Novemba 13, 2025 - Mkurugenzi wa Halmashauri ya Manispaa ya Geita, Ndugu Yefred Myenzi, amefanya ziara ya ukaguzi wa miradi ya maendeleo akiwa ameambatana na wakuu wa idara na vitengo mbalimbali. Miradi iliyotembelewa ni ile iliyopewa fedha kutoka Serikali Kuu pamoja na fedha za mradi wa BOOST, yenye jumla ya thamani ya Shilingi 1,089,470,000.
Katika ziara hiyo, Mchumi wa Manispaa, Bi. Annastazia Richard, amesema kuwa ziara imewezesha timu ya menejimenti kujionea hatua mbalimbali za utekelezaji wa miradi na kufuatilia kama utekelezaji unakwenda sambamba na mpango kazi uliopangwa.
Afisa Elimu Msingi wa Manispaa ya Geita, Mwl. Sostenes Mbwilo, amesema miradi 9 ya BOOST iliyotembelewa ipo katika hatua nzuri ya ujenzi, ambapo mingi imefikia zaidi ya asilimia 90 ya utekelezaji.
Kwa upande wake, Mganga Mkuu wa Halmashauri ya Manispaa ya Geita, Dkt. Sunday Mwakyusa, amesema miradi ya sekta ya afya iliyokaguliwa ipo katika hali nzuri, na ana matumaini kuwa yote itakuwa imekamilika ifikapo tarehe 30 Novemba 2025.
Akihitimisha ziara hiyo, Mkurugenzi wa Manispaa ya Geita Ndugu Yefred Myenzi amewapongeza wasimamizi wote wa miradi kwa kazi nzuri wanayoifanya na kuwataka mafundi waliokabidhiwa kazi kuhakikisha wanakamilisha ujenzi kwa wakati. Pia ametoa maelekezo kwa vitengo husika kuanza utaratibu wa fidia katika maeneo ya miradi yanayohitaji taratibu hizo.
Aidha, amefafanua kuwa kiasi cha zaidi ya Shilingi bilioni 3.4 kimetengwa na kuelekezwa kwenye miradi mbalimbali ya maendeleo ndani ya manispaa. Amesisitiza kuwa kila robo ya mwaka, Halmashauri itaendelea kuelekeza fedha kwenye miradi ya maendeleo kwa ajili ya kuboresha maisha ya wananchi.
Mkurugenzi Myenzi ameahidi kuwa menejimenti itaendelea na ziara za mara kwa mara kufuatilia maendeleo ya miradi na kuhakikisha inatekelezwa kwa ubora na viwango vilivyokusudiwa, akisisitiza kuwa lengo kuu ni kuzalisha miradi bora yenye tija kwa wananchi wa Geita.
Geita Tanzania
Sanduku la Posta: P.o Box 384 Geita
Namba ya Simu: 0282520437
Mobile:
Barua pepe: td@geitatc.go.tz
Hatimiliki 2017 Halmashauri ya Mji Geita . Haki zote zimehifadhiwa